Tuesday 28 February 2017

MVUA KUBWA YANYESHA NAKUSABABISHA VIFO VYA WATU...........HII LEO


WATU wanne wa Kijiji cha Namkongo Kata ya Mipingo Wilaya ya Lindi, wamefariki dunia baada ya kusombwa na maji kufuatia mvua zinazoendelea kunyesha mkoani humu. Tukio hilo lilitokea Alhamisi iliyopita.
Diwani wa Kata ya Mipingo, Saidi Naomari, aliwataja waliofariki dunia katika tukio hilo kuwa ni Abdulrahman Mtopwa, Zainabu Nangungwa, Nuru Machungira na Khadija Machungira, wakazi wa kijiji cha Namkongo.
Katika siku hiyo, Juma Mbilinga na Mohamed Limuhu wa kijiji cha Mnyangara, na Swabaha Ahamad na mkewe Somoe Myemba wa kijiji cha Matapwa walinusurika kwa kupanda juu ya mti na baadaye kuokolewa na majirani.
Diwani huyo alisema miili ya watu watatu ilipatikana na kuzikwa, na kwamba mvua zinazoendelea kunyesha hivi sasa zimesababisha mito na mabonde kujaa maji.
Naomari alisema mvua hizo licha ya kusababisha vifo, pia zimeleta hasara kwa kusomba mifugo, kuharibu mazao mashambani, kubomoa nyumba na kuharibu miundombinu ya mawasiliano ya barabara kati ya kata hizo na maeneo mengine.
“Bado tathmini kamili ya mazao yaliyoharibiwa haijafanyika, lakini mbuzi saba kati ya 30 wa Mohamed Limuhu, walisombwa na maji,” alisema Diwani Naomari.
Alisema mawasiliano ya barabara kutoka Mipingo kwenda Mkwajuni na maeneo mengine ya Vijiji vya Nangoo, Mnyangara na maeneo mengine, yamekosekana kutokana na mvua hizo kubomoa madaraja na makalavati.
Mkuu wa Wilaya ya Lindi, Shaibu Ndemanga, alithibitisha kutokea kwa matukio na vifo hivyo.
Ndemanga alisema serikali ya wilaya ikishirikiana na mkoa, inaendelea na utaratibu kwa ajili ya kuwasaidia waliokumbwa na majanga hayo.


No comments:

Post a Comment